MWANDISHI WETU,DAR ES SALAAM
SHIRIKA la Bima la Taifa (NIC Insurance) limeendelea kutanua wigo wa huduma zake ambapo sasa huduma ya Bima ya COMESA inapatikana katika matawi yote yaliyopo kwenye mipaka yote yaTanzania.
Ifahamike kuwa COMESA ni Soko la Pamoja la nchi za ukanda wa Mashariki na Kusini mwa Afrika, likijumuisha nchi wanachama 13 ambazo ni Tanzania, Burundi, DR Congo, Djibouti, Eritrea, Ethiopia, Kenya, Malawi, Rwanda, Sudan, Uganda,, Zambia, na Zimbabwe.
Bima ya COMESA ni mahsusi kwa Watanzania wanaosafiri na vyombo vya moto kwenda nchi wanachama wa COMESA pasipo kuhitaji bima nyingine ya utatu ambayo ni ya lazima kisheria kwa vyombo vyote vya moto.
Akizungumza na Demokrasia juu ya Bima hiyo Ofisa Bima,Enid Zakayo amesema NIC Insurance ni wasimamizi wa utoaji huduma wa bima ya COMESA hapa nchini, ikiwa ni pamoja na kutoa fidia stahiki pindi mteja apatapo ajali na kusababisha uharibifu wowote wa mali au chombo cha moto kwa mtu wa tatu.
“Ili kupata bima hii,mteja anapaswa kutoa taarifa za safari yake, ni muda gani atakuwa nje ya nchi ili aweze kulipia gharama za bima yake kulingana na muda wa safari na matumizi ya chombo chake cha moto.
“Aidha Bima hii mteja anaweza kukata kuanzia siku 10 hadi mwaka mmoja, ambapo mteja atalipia Sh.5000 ya kadi(COMESA yellow card) na Sh.8000 kwa kila kiti cha abiria ikiwa ni gharama ya matibabu kwa abiria au mtu wa tatu atakaye husika katika ajali hiyo” amefafanua Ofisa huyo wa NIC Insurance
Zakayo amesema Bima ya COMESA itamsaidia mteja kutumia chombo cha moto akiwa kwenye nchi tajwa bila wasiwasi wowote.
Aidha ameongeza kuwa Bima hiyo ni muhimu sana na ina manufaa makubwa hivyo aliwataka Watanzania wanaosafiri kwenda nchi hizo kuchangamkia Bima hiyo.