NA JOHN MAPEPELE,WU HANI,CHINA
SERIKALI ya Tanzania imesisitiza dhamira yake ya kujenga sekta imara ya viwanda vya dawa na kuifanya nchi kuwa kitovu cha uzalishaji wa dawa kwa ukanda wa Afrika Mashariki na kwingineko barani Afrika, huku ikizidi kuvutia uwekezaji wa kimkakati kutoka China.
Akizungumza Julai 7,2026 katika kikao na viongozi wa kampuni ya Jointown Pharmaceutical Group nchini China, inayoongoza kwa uzalishaji wa madawa kwa upande wa makampuni binafsi nchini hapa, Waziri wa Afya,Mohamed Mchengerwa amesema Tanzania imejipanga kuendeleza Eneo Maalum la Kiuchumi la Dawa na Vifaa Tiba la Mloganzila, ambalo litakuwa kitovu cha uwekezaji katika uzalishaji wa dawa, malighafi za dawa (APIs) na vifaa tiba.
Amesema, eneo hilo limeboreshwa kwa miundombinu ya kisasa na linaunganishwa kwa urahisi na Bandari ya Dar es Salaam pamoja na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
Waziri Mchengerwa amebainisha kuwa Serikali iko tayari kushirikiana na Jointown katika kuanzisha uzalishaji wa malighafi za dawa, hatua itakayoongeza uwezo wa Tanzania kujitosheleza kwa dawa muhimu na kuiwezesha kuhudumia masoko ya kikanda.
“Ushirikiano kati ya Jointown na Bohari ya Dawa (MSD) unatarajiwa kuleta mageuzi katika mifumo ya ugavi, uhifadhi na usambazaji wa dawa nchini kupitia matumizi ya teknolojia na uzoefu wa kampuni hii kubwa hapa China katika usimamizi wa minyororo ya usambazaji duniani” amesema Mchengerwa
Aidha Mchengerwa amethibitisha Serikali inayoongozwa na Rais wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, inafuatilia kwa karibu uwekezaji wa dawa nchini na ameahidi ushirikiano wa Serikali kwa wawekezaji watakaochangia maendeleo ya sekta ya afya.
Katika kuonesha utayari wa Serikali, Waziri Mchengerwa amesema Tanzania ipo tayari kutenga maeneo ya kutosha kwa ajili ya uwekezaji wa uzalishaji wa malighafi za dawa, akieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya dhamira ya dhati ya kuharakisha uanzishwaji wa viwanda vya kisasa vitakavyozalisha dawa kwa matumizi ya ndani na kwa ajili ya soko la Afrika.

