NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM
MKAZI wa Goba jijini Dar es Salaam, Adam Ahmad, ameibuka mshindi wa pikipiki mpya aina ya TVS kupitia mnada wa kidijitali unaoendeshwa na kampuni ya PIKU, baada ya kushiriki kwa kuweka dau dogo la shilingi 1,000 mara kwa mara.
Pikipiki hiyo imeambatana na bima ya mwaka mzima pamoja na mshindi kuwekewa mafuta ya lita 30 kila mwenzi kwa muda wa mwaka mzima.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa zawadi hiyo, Adam amesema alianza kushiriki minada ya PIKU baada ya kuambiwa na rafiki yake ambaye tayari alikuwa mchezaji wa muda mrefu.
“Niliweka dau dogo la kipekee. Unanunua tiketi halafu unashiriki kwa kucheza mara nyingi. Mwisho wa siku nimejishindia pikipiki. Nimefurahi sana kwa sababu sasa itanisaidia katika biashara zangu za bodaboda,” amesema Adam.
Adam, ambaye ni dereva bodaboda kwa muda mrefu, amesema ndoto yake kubwa ilikuwa kumiliki pikipiki yake mwenyewe, jambo ambalo sasa limefanikiwa kupitia PIKU.
“Nilikuwa nanunua tiketi za shilingi 1,000 na kucheza mara kwa mara. Haijafika hata shilingi 50,000 lakini leo nimeshinda pikipiki. Namshukuru Mungu,” ameongea kwa furaha.
Aidha, Adam amewahamasisha vijana wenzake kujiunga na PIKU, akisisitiza kuwa mchezo huo unaendeshwa kwa uwazi na hauna ujanja ujanja wowote.
Kwa upande wake, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa PIKU, Barnabas Mbunda, amesema kampuni yao inalenga kusaidia Watanzania kiuchumi kwa kupitia minada inayoendeshwa kwa uwazi na kwa kufuata sheria.
“Leo tumetoa zawadi ya pikipiki aina ya TVS, ina bima ya mwaka mzima pamoja mshindi kupata nafasi ya kuweka mafuta mwaka mzima, pia yupo mshindi wa televisheni ya LG nchi 55 pamoja na router yenye intaneti kwa mwaka mzima.
Tunataka kurahisisha maisha ya watu kwa kuwapa fursa ya kushinda vitu vinavyoweza kuwainua kiuchumi,” amesema Mbunda.
Ameongeza kuwa mshindi wa pikipiki si tu amepewa chombo hicho, bali pia mafuta ya lita 30 kila mwezi kwa kipindi cha mwaka mzima pamoja na bima ya mwaka mzima.
“Tunafanya haya kwa nia ya kuwainua wananchi kiuchumi. PIKU ni kampuni halali, imesajiliwa na inafanya kazi kwa kufuata sheria zote za nchi,” amesisitiza Mbunda.
Kwa upande wake, Mkaguzi kutoka Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania, Joram Mtafya, amethibitisha kuwa PIKU inafanya kazi kwa mujibu wa sheria, na kila droo ya mshindi hufanyika mbele ya mwakilishi wa bodi hiyo.
“Kila droo lazima iwe na mwakilishi kutoka bodi yetu ili kuhakikisha taratibu zote zinafuatwa na mshindi anapatikana kihalali. Tunatoa wito kwa kampuni nyingine zinazofanya michezo ya kubahatisha kujisajili ili kuchangia mapato ya serikali,” amesema Mtafya.
Katika hafla hiyo, mshindi mwingine, Nasra Ally, ambaye alipata televisheni ya LG nchi 55, ameeleza furaha yake baada ya kuibuka mshindi huku akihamasishwa na wenzake kazini.
“Mwenzangu kazini alianza kucheza, tukawa tunashindana. Nakumbuka mtu wa kwanza kushinda alikuwa kutoka Zanzibar, ndipo nikasema kama yeye kaweza, kwa nini mimi nishindwe?
“Mchezo huu ni wa kweli, hakuna ujanja ujanja. Nawashauri watu wacheze ili nao wajishindie kama mimi nilivyopata TV. Rafiki yangu ambaye tulikuwa tunashindana alitamani kuja anisindikize, lakini amekosa muda,”.