NA MWANDISHI WETU,DODOMA
TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imewaasa watendaji wa uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye Magereza kwa Tanzania Bara na Vyuo vya Mafunzo kwa Tanzania Zanzibar kufanya kazi kwa weledi.
Wito huo umetolewa wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku tatu kwa watendaji hao ambayo yameanza leo Jumapili Juni 22 2025 mkoani Dodoma kwa Magereza sambamba na Unguja kwa Vyuo vya Mafunzo.
Akifungua mafunzo kwa watendaji hao yaliyofanyika mkoani Dodoma kwa watendaji wa Magereza, Tanzania Bara, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jacobs Mwambegele amesema Tume imewateua watendaji hao kutokana na weledi wao.
“Sina shaka kuwa kuteuliwa kwenu kunatokana na ujuzi, uwezo na weledi mlionao katika kutekeleza majukumu ya kitaifa likiwepo zoezi la uboreshaji wa Daftari ambalo ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025,” amesema Mwambegele.
Amewahakikishia watendaji hao kuwa kwenye mafunzo hayo ya siku tatu Tume itawapa ujuzi wa kutosha kwa nadharia na vitendo kuwawezesha kutekeleza jukumu lao kwa weledi.
Akifungua mafunzo kama hayo Kisiwani Unguja, Zanzibar kwa watendaji wa Vyuo vya Mafunzo, Makamu Mwenyekiti wa Tume, Jaji wa Rufani Mstaafu, Mbarouk Salim Mbarouk ametoa wito kwa watendaji hao kuvitunza vifaa vya uboreshaji wa daftari.
“Ninatoa wito kwenu kuhakikisha mnavitunza vifaa vyote vitakavyotumika katika zoezi la uboreshaji wa Daftari na kuzingatia maelekezo yote yatakayotolewa na Tume ili muweze kuyafanyia kazi kwa usahihi wakati wote wa utekelezaji wa zoezi hilo,” amesema.
Jaji Mbarouk pia amewahakikishia watedaji hao kuwa Maofisa kutoka Tume watakuwepo muda wote wa zoezi na kwamba endapo watapata changamoto ya aina yoyote wasisite kuwasiliana nao.
Kwa mujibu wa ratiba zoezi hilo la uboreshaji wa Dafatri kwenye Magereza na Vyuo vya Mafunzo linafanyika kwa siku saba kuanzia Juni 28 hadi Julai 04, 2025 ambapo watakaohusika ni mahabusu na wafungwa walihukumiwa kifungo chini ya miezi sita.