NA MWANDISHI WETU,DAR ES SALAAM
MASHIRIKA mawili makubwa yanayojihusisha na haki za kidijitali ya Paradigm Initiative (PIN) na Tech & Media Convergency (TMC) yametoa mapendekezo kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kurejesha kikamilifu upatikanaji wa Mtandao wa X (zamani Twitter) na kujitolea kwa intaneti iliyo wazi na inayopatikana kwa wote kabla, wakati, na baada ya uchaguzi.
Mapendekezo hayo yalitolewa Mei 29, 2025 jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa TMC Shirika linalojishughulisha na Maendeleo ya TEHAMA nchini Asha Abinallah kufuatia Serikali ya Tanzania kuzuia upatikanaji wa mtandao wa X (zamani Twiter) alipokuwa akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika baada ya kumalizika kwa warsha ya siku mbili ya “Digital Rights and Elections in Africa Monitor (DREAM)” Toleo la Tanzania, uliangazia vitisho vinavyojitokeza na vikwazo vinavyoendelea dhidi ya haki za kidijitali kuelekea Uchaguzi Mkuu 2025.
Abinallah alieleza wasiwasi wa mashirika hayo kuhusu hali ya haki za kidijitali na nafasi ya kiraia, hususan katika eneo la uhuru wa kujieleza, upatikanaji wa taarifa, na uhuru wa vyombo vya habari mtandaoni.
Alipendekeza pia TCRA Kuepuka kufuta au kuzima kwa hiari majukwaa ya vyombo vya habari mtandaoni na kuhakikisha uhuru wa kujieleza mtandaoni na nje ya mtandao, hasa kwa wanahabari, wanasiasa, na sauti za kiraia kama inavyolindwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Pamoja na hayo alipendekeza kutangaza taarifa za uchaguzi kwa njia rahisi kufikiwa na kwa lugha za kienyeji ambapo kwa upande wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (CHRAGG), aliitaka Tume hiyo kufuatilia hali ya haki za kidijitali wakati wa mchakato wa uchaguzi na kuripoti ukiukwaji kwa uwazi.
Kadhalika kwa kushirikiana na asasi za kiraia alipendekeza Tume hiyo ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kuongeza uelewa kuhusu matumizi bora ya mitandao.
Kwa upande wa Kampuni za Mawasiliano, ametakiwa kuhakikisha utulivu wa mitandao na uwazi kuhusu maagizo yoyote kutoka serikalini kwa kutoa taarifa kwa umma na kuchapisha ripoti za uwazi mara kwa mara kuhusu maombi ya serikali kuhusu maudhui au upatikanaji wa taarifa.
Alisisitiza tena dhamira yao ya kuendeleza mazingira jumuishi, shirikishi, na yenye kuheshimu haki katika matumizi ya kidijitali Tanzania inapojielekeza kwenye mojawapo ya nyakati muhimu zaidi za kidemokrasia katika historia yake.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Paradigm Initiative Gbenga Sesan alisema Mpango wa DREAM ni sehemu ya mradi wa bara zima unaoratibiwa na Paradigm Initiative kufuatilia, kuhifadhi kumbukumbu, na kujibu ukiukwaji wa haki za kidijitali katika vipindi vya uchaguzi.
Kwamba Toleo hili linajengwa juu ya jitihada zilizofanyika wakati wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka 2024 na linafanyika sambamba na Mkutano wa 2025 wa Utawala wa Mtandao Afrika (AfIGF).