NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM
VYOMBO vya Habari hapa nchini vimetakiwa kuheshimu tofauti ya maoni ya kila mtu kutokana na mawazo na misimamo ya kile anachokiamini hata kama sio sahihi .
Hili linatajwa kutokana na nchi yetu kuelekea katika kipindi cha Uchaguzi Mkuu mwaka 2025 ambapo katika jamii kuna watu wenye mitazamo mbalimbali kulingana na vipaumbele vyao ingawav vyombo vya habari vina fursa ya kutoa uelekeo kwa taifa.
Kadhalika vimetakiwa kuhakikisha kuwa vinabaki kuwa kioo cha jamii kisicho na doa la uzushi, chuki au upendeleo na kuendelea kuhimiza maelewano, uvumilivu wa kisiasa, na utamaduni wa kuheshimu tofauti za maoni.
Haya yameelezwa leo Jumatano Julai 9,2025 na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dotto Biteko jijini Dar es salaam wakati akifungua Mkutano wa Wadau Kujadili Mchango wa Sekta ya Habari katika kufanikisha Uchaguzi Mkuu
Sambamba na hilo Dk. Biteko amewaasa waandishi wa habari nchini kuwa walinzi wa ukweli, wajenzi wa amani na wachochezi wa uwajibikaji wa kisiasa.
“ Ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kuwa, waandishi wa habari katika kipindi chote cha mchakato wa uchaguzi wanabaki salama wao pamoja na mali zao.
” Aidha, Serikali, tutaendelea kulisimamia hili kwa nguvu zetu zote. Tutahakikisha kuwa, mnakuwa na mazingira salama, huru na rafiki wakati wote wa majukumu yenu, amesema Dk Biteko.
“Uchaguzi ni kipindi cha muda mfupi, tumuombe Mungu hata baada ya Uchaguzi tubaki kuwa Taifa moja lenye ustahimilivu na kila mmoja akitoka kwake aende kutafuta mkate arudi nyumbani kwa familia yake kukiwa na amani, sisi kupitia mkutano huu tuungane kuhakikisha Taifa letu linabaki salama. Sekta ya habari ni nyenzo muhimu katika kulinda na kudumisha amani katika kipindi chote cha uchaguzi,” amesisitiza Dk. Biteko.
Ameongeza kuwa kutokana na mazingira wezeshi kwa sekta hiyo ya habari Tanzania kwa sasa ina idadi kubwa ya vyombo vya habari ikilinganishwa na miaka iliyopita, ambapo kuna jumla ya magazeti 375, vituo vya redio 247, vyombo vya habari vya mtandaoni 355, blogs 72 na vituo vya televisheni 68, hivyo amevitaka vyombo hivyo kukumbushana wajibu wao na kuzingatia miiko na maadili ya taaluma yao na kuilinda tasnia yao kwa wivu mkubwa.
Kutokana na utafiti wa Taasisi ya REPOA (Research on Poverty Alleviation) mwaka 2022 unaonesha kuwa vyombo vya habari ndiyo chanzo kikuu cha taarifa za kisiasa kwa wananchi ambapo zaidi ya asilimia 76 ya wananchi hupata taarifa za kisiasa kupitia vipindi vya redio na televisheni.
Dk. Biteko ameviasa vyombo vya habari kutoa majukwaa ya mijadala ya kisera na kisiasa ambayo huwasaidia wapiga kura kufanya maamuzi sahihi kwa kusikiliza sera na ajenda za wagombea ikiwa ni pamoja na kuhamasisha ushiriki wa makundi yote katika jamii, yakiwemo wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
Aidha, amesema kuwa Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuhakikisha Sekta ya Habari na Utangazaji nchini inakua na kutoa huduma bora kwa weledi na kwa kuzingatia maadili ambapo Aprili 6, 2021 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk.Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo ya kuvifungulia vyombo vya habari vilivyokuwa vimefungiwa na pia kuvirejeshea leseni vyombo vya habari ambavyo vilikuwa vimemaliza adhabu zake ili viendelee na majukumu ya kuhabarisha jamii.
Amesema ni hatua ambayo inadhihirisha kuwa Serikali ya Dk. Samia inaendeleza dhana ya kuheshimu na kuipa kipaumbele sekta ya habari nchini ili Watanzania wapate habari sahihi.
” Serikali itaendelea kuthamini na kuenzi mchango wa sekta ya habari, aidha, katika kutekeleza kwa vitendo falsafa ya “4Rs” yaani Maridhiano (Reconciliation), Ustahimilivu (Resilience), Mageuzi (Reforms), na Ujenzi Mpya wa Taifa(Rebuilding) bado sekta ya habari inahitajika na mchango wake ni wa muhimu.”
Hatahivyo, Dk. Biteko amesema kutokana na matumizi makubwa ya teknolojia na mitandao ya kijamii sekta ya habari ina jukumu kubwa la kupambana na taarifa potofu na kuhakikisha kuwa jamii inapata taarifa sahihi kwa njia ya kidigitali kwa kutumia lugha ya staha, kuepuka uchochezi na kuripoti kwa usawa, vyombo vya habari huchangia katika kudumisha utulivu wa kitaifa.
Katika hatua nyingine Dk.Biteko ameipongeza Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC)kwa kazi wanayoifanya kuandaa uchaguzi wa mwaka 2025 na kusema kuwa ni Rais Samia angependa kuona uchaguzi unafanyika kwa haki na amani.
“ Ni matarajio yetu kuwa Tume itaendelea kushirikiana na vyombo vya habari kwa karibu, kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu taratibu zote za uchaguzi. Ushirikiano huu ni nguzo muhimu ya kuimarisha imani ya wananchi kwa mchakato wa uchaguzi.” amesema Dk.Biteko
Pamoja na ufunguzi wa mkutano huo, Dk. Biteko amezindua rasmi Mfumo wa Kidigiti wa TAI – Habari wa kusajili na kutoa ithibati kwa waandishi wa habari ambao unasimamiwa na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari ambapo hadi sasa Bodi hiyo imesajili waandishi wa habari zaidi ya 2900 kupitia mfumo huo ambao unachakata taarifa zote muhimu za mwandishi wa habari na kisha kumpatia mwandishi wa habari kitambulisho cha kidigiti (Digital Press Card.)CYOMBO VYA HABARI VIHESHIMU TOFAUTI YA MAONI
Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Prof. Palamagamba Kabudi amesema kuwa kupitia mkutano huo wa wadau wa sekta ya habari wanalenga kuweka msingi madhubuti wa ushirikiano kati ya Serikali, vyombo vya habari, asasi za kiraia, taasisi za usalama na taasisi huru kama Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, ili kulinda amani, kuhimiza usawa wa fursa kwa vyama vyote vya siasa, na kuruhusu wananchi kupata taarifa za msingi zitakazowawezesha kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kuchagua viongozi wao.
“Tunafahamu kuwa uchaguzi ni tukio nyeti. Ni kipindi ambacho jamii inakuwa na matarajio makubwa ya kupata taarifa zilizo sahihi, kwa wakati na zisizo na upendeleo. Ndiyo maana mkutano huu pia umehusisha vyombo vya ulinzi na usalama, ili kwa pamoja tuhakikishe kuwa waandishi wa habari wanafanya kazi katika mazingira salama, bila vitisho wala bugudha. Ushirikiano baina ya Jeshi la Polisi na vyombo vya habari ni jambo la msingi na tunalipa kipaumbele katika mjadala wetu wa leo,” amesema Prof. Kabudi.
Naye, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Mhe. Albert Chalamila amesema wataendelea kushirikiana na vyombo vya habari ili kuhakikisha wanapata taarifa sahihi kutoka ndani ya Mkoa huo na Wilaya zake na kuhabarisha wananchi.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema kuwa Wizara yake kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) wameona umuhimu wa kuungana katika mkutano huo kwa lengo la kujadiliana ili kuhakikisha sekta ya habari inashiriki Uchaguzi Mkuu kwa mwaka 2025 kwa weledi.
“Mwaka huu tunashiriki Uchaguzi Mkuu tukiwa tumesimamia weledi, tumeanza kuendesha taaluma yetu kitaalamu na sasa tuna mfumo wa kidigiti wa kusajili na kutoa ithibati kwa waandishi wa habari,” amesema Msigwa.