NA MWANDISHI WETU,UJERUMANI
BALOZI wa Tanzania nchini Ujerumani, Hassani Mwamweta anaongoza ujumbe wa wakulima na wafanyabiashara kutoka Tanzania unaoshiriki Maonesho ya Kimataifa ya Matunda na Mbogamboga ya Fruit Logistica 2026 yanayofanyika Berlin kuanzia Februari 03 hadi 06, 2026.
Ujumbe huo unajumuisha Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA),Saleh Mohamed unatumia maenesho hayo kupata fursa ya kutanua masoko kwa kuongeza masoko mapya, kuongeza mtandao wa wafanyabiashara na kujifunza maarifa mapya kuhusu kilimo-biashara.
Kampuni zaidi ya 40 kutoka Tanzania kwa kushirikiana na Taasisi za TAHA, Mamlaka ya Udhibiti Nafaka na Mazao mchanganyika (COPRA) na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) wameshiriki Maonesho hayo ambayo yamehudhuriwa na kampuni zaidi ya 2600 kutoka nchi 151 duniani.
Fruits Logistica ni Maonesho ya Kimataifa ya Matunda na Mbogamboga ambayo huwaleta pamoja wakulima, wasambazaji, wanunuzi, wasafirishaji na wadau mbalimbali katika mnyororo wa usambazaji wa matunda na mbogamboga kutoka duniani kote.






