NA MWANDISHI WETU, YOKOHAMA,JAPAN
WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) amewasili jijini Yokohama, Japan kumwakilisha Dk.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkutano wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Afrika (Tokyo International Conference on African Development-TICAD 9) ambao unafanyika kwa ngazi ya Wakuu wa Nchi na Serikali wa Nchi Wanachama wa Umoja wa Afrika na Japan kuanzia tarehe 20-22 Agosti 2025.
Waziri Kombo amepokelewa na Hideaki Harada , Balozi wa Zamani wa Japan nchini Namibia ambaye amekasimiwa jukumu la kumpokea Kiongozi wa Ujumbe wa Tanzania; Balozi wa Tanzania nchini Japan, Baraka Luvanda ambaye ameambatana na Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia, Felista Rugambwa na Maafisa Wandamizi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Wizara ya Fedha na Ubalozi wa Tanzania nchini Japan.
Waziri Kombo pamoja na kushiriki mkutano huo atafanya mazungumzo na Takeshi Iwaya, Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan; Ando Naoki, Makamu wa Rais wa JICA; viongozi mbalimbali wa Serikali na Taasisi wa Japan; Wakuu wa Taasisi na kampuni za uwekezaji wa Japan kwa ajili ya kuhamasisha uwekezaji, biashara na utalii hapa nchini.